HAKI ELIMU UDAHILI WA SHULE ZA MSINGI UMEFIKIA KIWANGO KILICHOWEKWA KIMATAIFA CHA ASILIMIA 96.9% KWA WATOTO WALIOANDIKISHWA SHULE

Na Humphrey Shao, Globu ya Jamii

Tasisi isiyo ya kiserikali inayojishughulisha na tafiti katika masuala ya elimu nchini ya Haki elimu imemwaga sifa kwa serikali ya awamu ya tano kwa jisni ilivyoweza kuboresha sekta ya elimu kwa kipindi chake cha miaka mitatu iliyokaa madarakani tangu Rais Dk John Pombe Magufuli achaguliwe.

akizungumza na Waandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo wakati wa mapitio ya bajeti ya Wizara ya elimu ya mwaka 2019/2020 Mkurugenzi wa Shirika la Haki Elimu Dk.John Kalaghe amesema kuwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 unakamilisha kipindi cha miaka mitatu ya serikali ya  Awamu ya Tano  chini ya Rais John Pombe Magufuli  Miradi mikubwa ya maendeleo ya kiuchumi na kijamii imeanzishwa na inaendelezwa katika awamu hii. 

"Ukiitazama  sekta ya elimu  ongezeko la udahili  wa wanafunzi katika ngazi zote za elimu ni mojawapo ya mafanikio makubwa yaliyochagizwa na serikali ya Rais John Pombe Magufuli.  Udahili  wa watoto katika shule za msingi umeongezeka kwa 17% kutoka wanafunzi 8,639,202 mwaka 2016 hadi wanafunzi 10,111,255 mwaka 2018 (AJESR) 2018. Vivyo hivyo, kumekuwa na ongezeko la 12.6% ya wanafunzi katika shule za sekondari kutoka wanafunzi 1,908,857 mwaka 2017 hadi 2,148,466 mwaka 2018"alisema Dk Kalage.

amesema Udahili  katika shule za msingi umefikia karibu na kiwango kilichowekwa  kimataifa kwa asilimia 96.9% (kwa watoto wote walioandikishwa bila kuzingatia umri) na asilimia 84% (kwa watoto walioandikishwa wakiwa na umri sahihi wa kuanza shule). Zaidi ya 70% ya wanafunzi wote wanaomaliza darasa la saba wanaendelea na elimu ya sekondari. Mafanikio haya tunayoyaona yamechangiwa na uamuzi wa Serikali ya Awamu ya Tano wa  kuondoa ada katika elimumsingi.

ametaja kuwa licha ya mafanikio haya Lakini mazuri, bado kuna changamoto kadhaa ambazo zinaikabili sekta ya elimu. Changamoto hizi has ni zile  zinazosababishwa na upungufu wa fedha zinazotengwa na zinazopelekwa katika sekta hii. Kwa mfano, wakati udahili wa wanafunzi umeongezeka kwa wastani wa 17% kama ilivyoelezwa hapo juu, idadi ya shule imeongezezeka  kwa 1% tu kwa shule zote za msingi na sekondari tangia mwaka 2016. Ripoti ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) ya mwaka wa fedha 2016/17, inaonesha upungufu wa 85% ya madarasa kwa shule za msingi, 83% kwa mashimo ya choo, 66% kwa nyumba za walimu  na 14% kwa madawati. Aidha, shule za sekondari zina upungufu wa 52% ya madarasa, 84% ya maabara, 86% ya madawati, 85% ya nyumba za walimu na vilevile 88% ya mabweni na 53% ya mashimo ya choo. Jambo hili linashtua sana.

amesema HakiElimu tukiwa mojawapo ya wadau muhimu katika sekta ya elimu,  tunalo jukumu la kuishauri serikali pamoja na bunge na kupendekeza njia sahihi za kufikia malengo ya mipango ambayo serikali imeweka ili kufanikisha elimu bora kwa wote. Wakati huu ambapo  wabunge na wizara zinakaa kwa ajili ya kupanga bajeti kwa mwaka wa fedha 2019/20, HakiElimu inatumia fursa hii kutoa mapendekezo ya maeneo ambayo tunadhani ni muhimu  kuzingatiwa kama ifuatavyo:

       Kuongeza  bajeti ya sekta ya elimu:  Katika vipindi vitatu vya miaka ya fedha iliyopita, bajeti ya elimu  imekuwa ikishuka kwa tabribani asilimia moja kila mwaka.  Mathalani mwaka 2016/17 bajeti ilikuwa  Tsh bilioni 4,770 lakini ikashuka hadi kufikia Tshs bilioni 4,706 katika mwaka wa fedha 2017/18 na mwaka 2018/19 bajeti iliyoidhinishwa ilishuka zaidi  hadi kufikia  Tshs  bilioni 4,628.   Katika hali ya kawaida  tungetegemea bajeti ya sekta ya elimu ingepanda ili kukidhi mahitaji ya ongezeko la wanafunzi  wanaodahiliwa na utekelezaji wa elimumsingi bila ada. Kielelezo kifuatacho  kinaonesha mwenendo wa bajeti kwa miaka mitatu iliyopita mfululizo.
      

Uwiano kati ya bajeti ya sekta ya elimu na bajeti kuu ya serikali umeshuka na kupungua chini ya viwango vinavyokubalika kikanda na kimataifa, vikiwamo viwango vilivyowekwa na Tamko la Incheon ( 2015) ambalo linazitaka nchi za kusini mwa Jangwa la Sahara kutenga 20% ya bajeti ya serikali kwenda sekta ya elimu. Uwiano wa bajeti ya elimu kwenye bajeti ya serikali (ukijumuisha deni la taifa) umepungua kutoka 16.1% kwa mwaka 2016/17 hadi 15% kwa mwaka 2017/18 na kushuka zaidi hadi kufikia 14% kwa mwaka 2018/19.  Kwa  kuzingatia ongezeko la bajeti ya taifa katika   miaka mitatu na kama serikali ingetenga walau 20% kwa sekta ya elimu,  bajeti ya sekta ya hii  ingeongezeka kwa jumla ya Tshs bilioni 4,666.

Kama kiwango hiki kingepangwa na kutolewa kingepunguza kwa kiasi kikubwa changamoto za miundombinu tulizozitaja awali.
HakiElimu inaishauri serikali, wizara husika na wabunge kuchagiza ongezeko la bajeti na uwiano wa bajeti ya sekta ya elimu na ule wa bajeti ya serikali kufikia 20%.


  Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI, Selemeni Jafo, alitoa ahadi ya kupeleka kiasi cha Tsh 29 bilioni kwa ajili ya miundombinu katika shule za kidato cha tano na sita. Fedha hizo zililenga kujenga madarasa 478 na mabweni 269 kwa ajili ya wanafunzi 21,808 waliokuwa wanatarajia kujiunga na kidato cha tano lakini hawakuweza kufanya hivyo kwa sababu ya upungufu wa madarasa. Mhe. Jafo, alitoa miezi miwili kwa serikali za mitaa kukamilisha ujenzi  wa miundombinu hiyo. Je, fedha hizo zilipelekwa? Na kama jibu ni ndiyo, je madarasa yaliyotegemewa yalijengwa? Na, je wanafunzi walianza shule katika kipindi stahiki? Majibu haya yatawasaidia wabunge na jamii kushauri ipasavyo.

amesema HakiElimu inatambua na inaipongeza serikali kwa uamuzi wa kufuta kodi ya ongezeko la thamani (VAT) katika taulo za kike, uamuzi uliofanyika katika bajeti ya mwaka 2018/19. Uamuzi huu ulichukuliwa kwa ajili ya kutatua changamoto ya muda mrefu ya wanafunzi wa kike kushindwa kuhudhuria shule kwa siku 2 hadi 3 kila  mwezi kwa sababu tu wanashindwa kukabiliana ipasavyo na namna ya kujihifadhi wakati wa siku za hedhi kwa kutokuwa na uwezo wa kununua taulo za kike. Kuondoa kodi kulitegemewa kungepunguza bei ya taulo za kike na kuzifanya ziweze kununuliwa kiurahisi na watoto wanaotoka katika familia duni.

" Hata hivyo, utafiti mdogo uliofanywa  na HakiElimu katika soko la bidhaa na kwa wanafunzi wa kike unaonesha kuwa kuna muitikio mdogo na sehemu zingine hakuna utekelezwaji kabisa wa tamko hili la serikali. Katika maduka mengi bei ya wastani ya taulo za kike ni ile ile ya shilingi 2,000/- ambayo familia duni nyingi haziwezi kuimudu. Jambo hili linakatisha tamaa sana siyo tu kwa wanafunzi wa kike bali hata kwa serikali."

amesema Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Mhe. Ummy Mwalimu, aliwasilisha masikitiko yake tarehe 15 Februari 2019 baada ya kugundua kuwa taulo za kike zinauzwa katika bei ambazo walio na maisha duni hawawezi kuzimudu. Alisema kuwa ameandika barua kwa Waziri wa Fedha na Waziri wa Viwanda na Biashara kuwasilisha masikitiko yake. Ni matumaini yetu kuwa wizara itafuatilia suala hili.  Pamoja na  hatua hii HakiElimu tunapendekeza serikali iangalie  uwezekano wa  kufanikisha upatikanaji wa taulo za kike moja kwa moja mashuleni kama ambavyo inafanyika kwenye baadhi ya nchi jirani.
       

 alimaliza kwa kusema kuwa matumaini yao  kuwa ushauri na maoni ya shirika hilo pamoja na wadau wengine utazingatiwa ili kuinua ubora  elimu nchini  na hivyo kuchangia  katika kufikia malengo ya Taifa ya kuwa na uchumi wa  kati ifikapo mwaka 2025.

 Mkurugenzi wa Shirika la Haki Elimu Tanzania, Dk. John Kalage akizungumza na Waandishi wa Habari juu ya tamko la Tasisi yake kwa Wizara ya Elimu katika Uchambuzi wa bajeti ya Wizara hiyo kwa mwaka wa Fedha wa 2019/2020
Mmoja ya Wakurugenzi wasaidiz wa Shirika la Haki elimu nchini Godfrey Boniventure akifafanua jambo kwa Waandishi wa Habari juu ya Uchambuzi wa bajeti hiyo.
Sehemu ya Waandishi wa habari wakimsikiliza Mkurugenzi wa Shirika la Haki elimu Nchini,Dk John Kalage

Post a Comment

Previous Post Next Post