NDEJEMBI AITAKA NHC KUJENGA NYUMBA BORA KWA BEI NAFUU

WAZIRI wa Ardhi,Nyumba na Maendeleo ya Makazi,Deogratius Ndejembi ametoa maelekezo kwa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) kuhakikisha wanafata malengo ya shirika ya mwaka 1962,yaliyowekwa na Baba wa Taifa Hayati Julius Nyerere ya kuhakikisha wanawajengea watanzania nyumba zilizobora na zenye bei nafuu.

Akizungumza jana jijini Dar es Salaam,wakati alipotembelea Shirika hilo kwa lengo la kujitambulisha kwa menejimenti ya shirika hilo,Ndejembi alisema shirika la NHC linaenda vizuri na kuingiza   faida ipasavyo.

Alisema katika kufanya majukumu yao NHC wanapaswa kutowasahau na kutowaacha nyuma  watanzania kwa kuhakikisha wanakuwa na  mipango mizuri ya kuhakikisha watanzania wanamiliki nyumba.

"Tunapaswa kuhakikisha  mtanzania anayejenga nyumba yake taratibu kwa fedha anazofanya  kazi au mjasiliamali aliyejipatia fedha zake ,tuhakikishe tunamrahisishie ndoto yake ya kupata nyumba kwa bei nafuu na iliyobora," alisema na kuongeza.

"Tunapaswa kutokusahau  malengo na maono ya Baba wa taifa Julius Kambarage ya kuhakikisha watanzania wanapata nyumba bora kama vile maono yake yalivyokuwa yanataka,"alisema.

Alisema  nyumba zinazojengwa zinapaswa kuwa za  bei nafuu kwa watu wote, kuwa za viwango bora na ziwe katika maeneo yanayofikika kwa urahisi  na isiwe kilometa 100 mbali na maeneo ya shughuli zao.

Waziri Ndejembi alisema mbali na hiyo shirika hilo linatakiwa kuhakikisha miradi wanayofanya inaonyesha thamani ya fedha.

"Hakikisheni miradi yetu kuwa na value of money ,niwaombe umakini katika miradi katika  hatua kwa hatua hususan katika manunuzi  ya maeneo kwenye mauzo na kuhakikisha  hakuna wizi,"alisema.

Aidha aliwapongeza kuwepo kwa mradi wa Samia Housing Scheme,kuwa na lengo la kujenga nyumba 5000, jambo hilo ni zuri hivyo ni jukumu la kuangalia maeneo ambayo yanauwezo wa kuwapata watu wengi zai ambao hawajafikia.

"Tusiache malengo yetu 1962 kuhakikisha tunajenga nyumba za kiwango kwa watanzania hasa kwa wale wa kipato cha chini,tuchanganye kwa jengo moja tunauza na nyingine tunapangisha kwa kipato cha chini nyumba ambazo ni za bei nafuu.

"Tukumbuke tunatengeneza mfumo ambao mtu atakuwa anauwezo wa  kulipa asilimia 10 au 20 ya nyumba alafu anaingia kwenye nyumba alafu anakuwa  analipa kodi kama kawaida ,baada ya hapo malipo haya yanayolipwa yanaingia katika ununuzi wake ambapo  baada ya miaka 5 au 10 nyumba inakuwa yake,"alisema .

Awali alipokuwa anawasilisha taarifa fupi  Waziri huyo kuhusu shirika lao ,Mkurugenzi  wa NHC ,Hamad Abdallah  alisema miongoni mwa jukumu lao kama NHC ni pamoja na kujenga nyumba za makazi na majengo mengine kwaajili ya kuuza na kupangisha.

Alisema shirika linajumla ya majengo 2872 yenye sehemu ya kupangisha zipatazo 20,349 ambapo rasilimali hizo zinaleta shirika kuwa na mtaji w Trilion 5.6.





Post a Comment

Previous Post Next Post